WAZIRI WA ELIMU PROF. NDALICHAKO AFICHUA SIRI NA MADUDU YA BARAZA LA TAIFA LA MITIHANI TZ (NECTA)


Waziri ashtushwa na lugha za walimu, Aahidi mabadiliko ndani ya mwaka.
Wakati shule zikifunguliwa leo kuanza muhula mpya wa mwaka 2016, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako, amefichua madudu kadhaa katika sekta hiyo.
Prof. Ndalichako aliyabaini hayo katika utafiti alioufanya kwa mwaka mmoja na kuapa kuwa atashirikiana na wenzake kufanya marekebisho makubwa katika sekta hiyo.
Prof. Ndalichako aliyewahi kuwa Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Mitihani (Necta) kwa miaka tisa kabla ya kuondoka mwaka 2012, alisema pamoja na mambo aliyobaini, usahihishaji wa kazi za wanafunzi, uadilifu wa walimu na wazazi ni viashiria vibaya kwa elimu nchini.
Alisema katika utafiti huo, imebainika kuwa wapo walimu hutumia lugha zisizofaa kwa wanafunzi, mfano ukidhihirishwa na maneno wanayoyaandika baadhi ya walimu kwenye madaftari ya wanafunzi wao baada ya kuwasahihishia mazoezi wanayowapa.





“Naamini maarifa yako kwenye daftari, jinsi mwalimu anavyosahihisha na comments zake zina msaada kwa wanafunzi, kwenye utafiti nilibaini wengi wanatoa comments zinazokatisha wanafunzi tamaa na lugha nyingine za mitaani zisizofaa, kwa mfano, kwenye shule moja nilichukua daftari la mtoto nikakuta mwalimu kamwandikia mwanafunzi ‘vizuri vizuri sana mrembo’… hii siyo sawa,” alisema Ndalichako.





Akieleza kuhusu chanzo cha utafiti huo, Waziri Ndalichako alisema kuwa aliamua kuomba likizo bila malipo (wakati akiwa NECTA) na kufanya utafiti huo baada ya kuona wanafunzi wengi wakifanya vibaya katika mitihani yao ya taifa huku baadhi ya wadau wakitoa majibu ya mkato kuwa mitihani ya baraza hilo ni migumu na kwamba haiendani na kile kilichomo kwenye mitaala ya elimu nchini.





“Mwanzoni, wakati watu wanalalamika kuwa mitihani ni migumu, nilikuwa najua siyo dhana sahihi kwa sababu walimu wanaofundisha watoto huko ndiyo waliokuwa wakiitunga (mitihani), na kila swali walilokuwa wakitunga walikuwa wakisema limetoka kwenye syllabus (muhtasari) gani, na mada husika iko ukurasa wa ngapi kwenye syllabus,” alisema Prof. Ndalichako na kuongeza:





“Ikafika mahali tukataka waseme kabisa hiyo mada ipo kwenye kitabu kipi, na ukurasa wa ngapi wa vitabu vile vilivyoidhinishwa kufundishia. Ndiyo maana watu walipokuwa wakilalamika tunatunga mitihani migumu, mara ipo nje ya mitaala, hizo kelele zilikuwa hazinisumbui kwa sababu nilikuwa najua mitihani yetu ni standard (ni ya viwango) na inatoka kwenye mitaala yetu,” alisema.





“Wakati mwingine nilikuwa nawaambia watu kama mitihani ni migumu basi tuanzie kwenye mitaala yetu. Na hilo lilikuwa ni tatizo la muda mrefu, nikaona nipate mwaka mmoja wa kukaa pembeni niangalie sababu hasa zinazofanya wanafunzi wasifanye vizuri,” alisema Prof. Ndalichako.





Alisema utafiti wake huo uliojikita kwenye mikoa ya Rukwa, Mbeya, Morogoro, Ruvuma, Mtwara, Lindi na Iringa, ulilenga pia kujua namna walimu walivyokuwa wakipata alama endelevu kwa wanafunzi, ambazo zilikuwa zikitumwa NECTA kwa ajili ya kutumika kwenye mitihani ya mwisho.





MADUDU


Akieleza kuhusu utafiti wake huo, alisema alibaini takribani sababu nane kubwa zinazosababisha wanafunzi wasifanye vizuri kwenye mitihani yao ya mwisho.





Alisema suala la uadilifu na kufuatwa kwa miiko ya taaluma ya ualimu ni moja ya sababu aliyobaini inachangia kufanya vibaya kwa wanafunzi katika mitihani yao.





“Walimu wengine ni wakali mno. Wanafunzi waliniambia kwamba wakati mwingine mwalimu akiuliza swali na mwanafunzi akakosea, mwalimu anamjibu vibaya na siku nzima huyo mwanafunzi hujikuta anakosa amani mbele ya wanafunzi wenzake,” alisema.





Akieleza zaidi, alisema jambo hilo hujitokeza hata kwenye madaftari ya wanafunzi ambako ndiko ilikobainika kuwa baadhi ya walimu huwaandikia wanafunzi kwa lugha kali na zisizofaa kutumiwa na walimu.





“Ngoja nikupe mifano ya lugha nilizokutana nazo kwenye daftari nilizokagua… ni pamoja na mwalimu mmoja kumwandikia mwanafunzi wake kuwa ‘andika mwandiko mzuri, unakuwa kama mtu ambaye hakunywa chai’,” alisema na kuongeza:





“Mwingine anaandika ‘dogo kaza buti’ … hii siyo lugha rasmi, ni ya mtaani… mwingine kaandika ‘dogo ongeza bidii utafeli’. Na yupo mwingine kamwandikia mwanafunzi ‘vizuri sana mrembo’. Sasa (iweje mwalimu) unamwandikia neno mrembo mwanafunzi? Hii inaonyesha jinsi tatizo la jinsi uadilifu linavyotupa changamoto,” alisema Ndalichako.





NINI CHA KUFANYA?


Akielezea kuhusu matatizo hayo, Prof. Ndalichako alisema amejipanga kuhakikisha kuwa kwa kushirikiana na wenzake, wanashughulikia matatizo ya aina hiyo kwa ukamilifu ili kuboresha sekta ya elimu nchini.





Alisema tayari ameshawaagiza wakaguzi wa shule kukagua madaftari ya wanafunzi wanapoenda shuleni na siyo kukagua majengo kama wanavyofanya sasa.





Alisema amebaini kuwa, baadhi ya wakaguzi hawajui ni nini kilicho kwenye madaftari ya wanafunzi kwa kuwa, hujikita zaidi kuangalia miundombinu ya shule badala ya kujua ni nini watoto wanafundishwa.
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.