Wananchi Wavamia Shamba la Sumaye na Kugawana


Wananchi zaidi ya 100, wakiwemo waliobomolewa maeneo ya mabondeni jijini Dar es Salaam, wamevamia shamba la Waziri Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye lenye ukubwa wa heka 33, lililopo Mji Mpya eneo la Mabwepande na kujikatia viwanja.

Sumaye ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa serikali ya awamu ya tano kati ya mwaka 1995 hadi 2005, amekiri wananchi kuvamia shamba hilo lakini alisema hana wasiwasi kwasababu ana hati za umiliki.

Aidha alisema atafuata mkondo wa sheria kuhakikisha wavamizi hao wanaondoka kwenye shamba lake.

Juzi mwandishi alishuhudia wananchi kadhaa wakiendelea kujenga nyumba za miti na wengine za matofali baada ya kujigawia kila mmoja eneo lake kwenye shamba hilo.

Musa Juma, aliyekutwa kwenye shamba hilo akijenga nyumba, alisema yeye ni miongoni mwa waathirika wa bomoa bomoa iliyofanyika Kinondoni Mkwajuni na kwamba amefika hapo baada ya mwenzao aliyemtaja kwa jina moja la Ema kuwaeleza kuwa kuna pori la Sumaye alilolitelekeza.

“Mwenzetu Ema alikuja kule bondeni tulikobomolewa na kutupa habari hiyo hivyo watu kama 100 tukaamua kuja na tukawakuta wengine tuliliona shamba hili likiwa ni pori kubwa ndipo tukaanza kujigawia vipande vipande,” alisema.

“Tumefanya kazi kubwa ya kulifyeka mpaka unaliona lipo katika hali hii, kazi haikuwa ndogo, tumekutana na nyoka wakubwa, ukishuka kule bondeni kwenye kingo za shamba utajionea mwenyewe jinsi pori hili lilivyokuwa.”
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.