Dk. Shein apiga marufuku mifungo mitaani Zanzibar.


Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein.
Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amelitaka Baraza la Manispaa Zanzibar kuimarisha shughuli za usafi wa mazingira, pamoja na kudhibiti mifungo kuingia katikati ya mji huo.
 
Dk Shein alitoa agizo hilo alipokuwa katika ziara ya kukagua miradi ya ujenzi inayogharamiwa kwa mkopo wa Benki ya Dunia ukiwamo ujenzi wa ukuta wa ufukwe wa Forodhani na mtaro wa maji machafu katika eneo la Mnazi Mmoja, Zanzibar jana.
 
Alisema wakati Zanzibar ikiwa katika mchakato wa kufikia sifa za kuwa jiji, lazima Baraza la Manispaa liongeze kasi ya usafi ikiwamo uhifadhi wa mazingira ya mji pamoja na udhibiti wa  majitaka visiwani humo.
 
Alisema haitoi picha nzuri  kuona mifugo bado inaonekana ikiranda mitaani wakati watendaji wametakiwa kuondoa tatizo hilo kwa muda mrefu sasa bila ya utekelezaji kuonekana.
 
“Lazima tuongeze jitihada za usafi wakati huu tukiwa katika kuelekea kufikia sifa na vigezo vya Zanzibar kuwa jiji,” alisema. 
 
Rais Dk. Shein alisema mradi wa kuboresha mji wa Zanzibar unaofadhiliwa na mkopo kutoka Benki ya Dunia una umuhimu mkubwa katika kuimarisha shughuli za usafi katika manispaa ya mji huo na miji ya Chakechake na Wete, Pemba.
 
Aliwataka watendaji kuhakikisha miradi hiyo inakuwa endelevu ili lengo lake liweze kuonekana la kuleta mabadiliko makubwa ya usafi wa mji huo.
CHANZO: NIPASHE
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.