Wabunge wachangia bajeti huku wakitangaza nia, wajue majina yao hapa



Suleiman Msuya, Dodoma

WABUNGE wa majimbo na viti maalumu wamechangia Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2015/16, kwa kutangaza nia za kugombea ubunge.
Hadi kufikia jana zaidi ya wabunge 20 kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) na upinzani wa kuchaguliwa na viti maalumu walitumia mjadala huo kutangaza nia.

Kangi Lugola

Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM) akichangia juzi pamoja na kuingia bungeni na bidhaa mbalimbali zinazozalishwa nje, aliweka bayana kuwa Mwibara bila Kangi mwana wa Lugola haiwezekani.
Lugola aliwataka wapigakura wake kutambua kuwa mafanikio ya huduma za kijamii kama maji, umeme, afya, barabara na zingine zimepatikana kupitia yeye, kwani miaka 55 ya uhuru hakukuwa na huduma hiyo.

Deo Filikunjombe

Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe (CCM), alisema miaka minne na nusu ambayo amewewatumikia wananchi wa Ludewa amefanya vizuri, hivyo anatarajia kurejea kuwaomba wamchague tena ili kukamilisha matarajio yao.

Filikunjombe alisema wakati akichukua jimbo hilo kulikuwa na vijiji vitatu pekee ndivyo vyenye umeme, lakini hadi kufikia leo vijiji 67 kati ya 77 vina umeme ikiwamo huduma ya miundombinu.

Ester Matiko

Kwa upande wake, Mbunge wa Viti Maalumu, Esther Matiko (Chadema), aliweka bayana kuwa anatarajia kugombea Jimbo la Tarime kupitia chama chake iwapo kitampitisha ili aweze kuwajibika moja kwa moja kwa wananchi wake.
Matiko alisema mbunge aliyekuwepo wa CCM, Nyambari Nyangwine ameshindwa kutekeleza mahitaji ya wananchi hivyo ni vema waweze kumpima kupitia Bunge kama anastahili kuwatumikia.

Ridhiwani Kikwete
Mbunge wa Chalinze, Ridhwan Kikwete (CCM), alisema kuwa anatarajia kurejea jimboni kuwaomba wananchi wamchague ili aweze kukamilisha mambo ambayo yamebakia.
“Mheshimiwa Mwenyekiti napenda kuwaambia wapigakura wangu wa Chalinze mchango huu kwani ni wa mwisho kwa Bunge hili ila natarajia kurudi tena kuwaomba niendelee kuwatumikia, kwani bado kuna mambo ambayo yamebakia hatujayatekeleza,” alisema Ridhiwani.
Akichangia bajeti hiyo alisema CCM ndiyo chama pekee ambacho kimeweza kuwafikisha Watanzania katika hali ya sasa ya mafanikio.
Ridhiwani alisema kumekuwa na sera ya afya kwa walemavu ya kutibiwa bure, lakini bado hawapati huduma hiyo. Pia, alioomba Serikali kuangalia uwezekano wa kujenga Hospital ya Chalinze ili iweze kusaidia kutoa huduma kwa wakazi wa jimbo hilo.

Ester Bulaya

Kwa upande wake, Mbunge wa Viti Maalumu, Esther Bulaya (CCM) ametangaza rasmi kugombea Jimbo la Bunda na kusema waliosema amepooza si kweli ni mzima wa afya.
Bulaya alisema alikuwa akiumwa, lakini kukawa na uvumi kuwa amepooza jambo ambalo si la kweli na kwa sasa ni mzima wa afya.
“Nimepona na nitasimama kugombea ubunge Jimbo la Bunda, maombi yenu yamefanya kazi na sasa nipo tayari kugombea,” alisema Bulaya.
Akichangia bajeti hiyo, mbunge huyo alisema kumekuwa na matumizi makubwa ya dola za Marekani hapa nchini kuliko shilingi ya Tanzania.
Bulaya alisema hivi sasa baadhi ya Watanzania wanajivunia kutumia dola katika kuwalipia watoto wao shule na hata katika malipo mbalimbali katika hoteli.

“Miaka ya nyuma akinamama wajasiriamali waliokuwa wakienda China kununua bidhaa mbalimbali wakiwa na dola walikuwa wakija na mizigo ya kutosha, lakini hivi sasa hakuna.

“Hivi sasa kila ukitembea hatua moja mbili unakutana na duka la kuuza fedha za kigeni hivi kweli uchumi wetu utapanda kupitia shilingi yetu lazima kufanya jambo hapa,” alisema.


Amina Mwidau

Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Mwidau (CUF), alisema anatarajia kugombea Jimbo la Pangani, kwani kila dalili za kushinda zipo na uwezo aliounesha katika bunge hili ni sababu ya kushinda.

Mwidau ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Hesabu za Serikali (PAC), alisema wananchi wa Pangani wanahitaji mabadiliko ambapo CCM haiwezi kuyaleta tena.

“Napenda kutumia nafasi hii kueleza kuwa naenda kuchukua fomu kupitia CUF, kwenda kukomboa Jimbo la Pangani na huo ndio mwendo wa Ukawa,” alisema.

Kuhusu bajeti, alisema kitendo cha kuongeza tozo kwenye mafuta ya taa, diseli na petroli ni aibu kwa Serikali kwani wananchi wa vijijini ndio wataumia zaidi.
Mbunge huyo alisema kila kona ya bahari ya Tanzania kuna bandari feki ambazo zinaingiza mizigo kwa njia ya magendo, hivyo kukosesha Serikali mapato.

John Lwanji

Kwa upande wake, Mbunge wa Manyoni Magharibi, John Lwanji (CCM), alisema miaka 10 ambayo amekuwa mwakilishi wao imekuwa ya mafanikio na kwamba atarejea kuwaomba wampe nafasi tena ya kukamilisha yaliyobakia.

Lwanji alisema kwa kipindi hicho Manyoni Magharibi, ilikuwa iko nyuma kimaendeleo kwa miaka mingi ila uwepo wake kumekuwa wa mafanikio makubwa ya kuwepo kwa miradi ya  maji, umeme, barabara na huduma zingine za msingi.

Abdul Aziz Abood

Kwa upande wake, Mbunge wa Morogoro Mjini, Abdul Azizi Abood (CCM), aliweka bayana kuwa anatarajia kurejea kwa wananchi wa Morogoro kuwaomba tena nafasi hiyo kupitia CCM, kwani ameweza kutekeleza ilani ya chama kikamilifu.

Alisema jitihada zionazofanywa na Ukawa haziwezi kufanya lolote katika jimbo hilo, kwani aliyoyafanya yanaonekana na kuahidi kuwa watashinda kwa kishindo.

Kuhusu bajeti aliitaka Serikali kujikita katika kuhakikisha kuwa viwanda vinafanya kazi, kwani bila kuwepo kwa viwanda ni dhahiri kuwa uchumi utashuka na shilingi.

Alitolea mfano viwanda vya mafuta ambapo alisema kuwa pamoja na juhudi za wakulima nchini kulima mazao ya mafuta bado Serikali imekuwa ikiruhusu uingizaji wa mafuta kutoka nje.

Susan Lyimo

Mbunge wa Viti Maalumu, Suzan Lyimo (Chadema), ametangaza nia ya kugombea Jimbo la Kinondoni, kupitia chama chake hiyo ikiwa ni baada ya kuwakilisha mkoa huo kupitia viti maalumu akiamini kuwa ni wakati wake wa kuwa mwakilishi wawananchi wa jimbo hilo linaloongozwa na Iddi Azzan.

Abia Nyabakari

Akichangia bajeti hiyo, Mbunge wa Viti Maalumu, Abia Nyabakari (CCM), alisema anatarajia kwenda kugomnbea Jimbo la Buyungu ambalo linaongozwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji na Uwezeshaji, Mhandisi Christopher Chiza.

“Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumuambia Mwenyekiti wa CCM, Wilaya ya Buyungu kuwa nakuja kugombea ubunge katika jimbo hilo naomba aniunge mkono,” alisema Nyabakari huku akipigiwa makofi.

Seleman Bungara

Mbunge wa Kilwa Kusini, Seleman Bungara (CUF), alisema anagombea tena jimbo hilo na CCM wasitarajie kupata chochote, kwani wameshindwa kufanya ambayo waliahidi kwa wananchi akitolea mfano barabara ya kilometa 4.5 ya lami imeshindikana kwa miaka mitano kujengwa.

Dustan Kitandula

Akichangia katika bajeti hiyo ya Wizara ya Fedha, Mbunge wa Mkinga, Dustan Kitandula (CCM), aliwataka wananchi wa jimbo lake kumpa nafasi nyingine ya miaka mitano ili aweze kutekeleza yale yote ambayo walikubaliana kuyakamilisha.

Kitandula alisema wapo watu ambao wanajipitisha jimboni humo ila kinachotakiwa ni kuwapuuza, kwani hawana jipya ambalo wanaweza kulifanya tofauti na yeye ambaye wameanza naye.

Herbet Mtangi

Hali kama hiyo ilijitokeza kwa Mbunge wa Muheza, Herbert Mtangi (CCM), alisema anatarajia kurejea kuomba ridhaa ya wananchi wa jimbo hilo, hivyo wakiamua kumrejesha atakuwa tayari kuwatumikia.

Salum Barwany

Mbunge wa Lindi Mjini, Salum Barwany (CUF), aliweka bayana kuwa atagombea huku akitoa tahadhari kwa CCM, kuangalia mtu ambaye wanataka kumuweka, kwani ataumbuka na kuwa aibu ndani ya chama hicho na mgombea huyo.

Wabunge wengine ambao wametumia bunge kutangaza nia ya kurejea kuomba kura  na majimbo yao katika mabano ni Dk. Athuman Mfutakamba (Igalula, CCM), Seleman Jafo (Kisarawe, CCM), Dk. Faustine Ndungulile (Kigamboni ,CCM), Murtaza Mangungu (Kilwa Kaskazini, CCM), Haman Yusuph Masauni (Kikwajuni, CCM), Aliko Kibona (Ileje, CCM), mawaziri ni Waaziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi (Isamini, CCM), Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe (Mwanga, CCM).
chanzo:gazeti la jambo leo 19 juni 2015
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.