MADENGE AWATAKA WAISLAMU KUIGA MBINU ZA WAKRISTO KUCHANGIA MAENDELEO YA DINI YAO

Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Mahamudu Madenge (kushoto) akikata utepe kuzindua rasmi mpango mkakati wa miaka mitatu (2015-2017) wa taasisi ya kiislamu ya mjini Iringa ya Dhi-Nureyn Islamic Foundation katika hafla iliyofanyika juzi mjini Iringa. Wengine ni Kaimu Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Abubakari Chalamila (katikati) na Katibu mtendaji wa taasisi hiyo, Elm Shamsi
Akipewa zawadi baada ya kuuzindua mpango huo
Baadhi ya waumini walioshiriki uzinduzi huo

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Mahamudu Madenge amewasihi waumini wa dini ya kiislamu nchini kote kutumia mbinu za wakristo kuchangia shughuli zake za maendeleo badala ya kuendelea kuzilalamikia changamoto zao kwa mamlaka au watu wasiohusika.

Aliyasema hayo mjini Iringa jana, mbele ya waumini wa dini hiyo walioshiriki uzinduzi wa mpango mkakati wa mwaka 2015 hadi 2017 wa taasisi ya kiislamu ya Dhi Nureyn Islamic Foundation yenye makao yake mjini hapa.

Katibu Mtendaji wa taasisi hiyo, Elm Shamsi aliyataja malengo ya mpango mkakati huo kuwa ni pamoja na kuondoa utegemezi kwa kujitafutia kipato kutokana na rasilimali chache walizonazo, kuitangaza taasisi ndani na nje ya nchi, na kusambaza elimu ya dini.

Mengine ni kutoa huduma bora za afya katika vituo vyake vya kutolea huduma, kuongeza kiwango cha ufaulu katika shule zake, kuboresha huduma kwa watoto yatima wanaolelewa katika vituo vyao na kuwasaidia vijana kujipatia ajira kwa kuwapa stadi za maisha kupitia vyuo vya ufundi.

Huku akiichangia Sh Milioni moja taaasisi hiyo, Madenge alisema maendeleo ya dini hiyo ni kama yanasuasua kwasababu baadhi ya waumini wake wanasubiri yaletwe au yachangiwe na watu wengine.

Akitoa mfano wa jinsi wakristo wanavyoshiriki katika kuiendeleza dini yao, Madenge alisema katika harambee zao za mara kwa mara za ndani na nje ya makanisa yao, wapo wanaoweza kununua chupa ya maji ya Sh 500 hata kwa Sh Milioni moja ili mradi kinachokusanywa kina lengo kufanikisha maendeleo ya dini hiyo.

“Kwa mfano hapa Iringa, dini hii ina watu wenye uwezo sana lakini ni mara chache sana kuwaona wakishiriki au kuchangia shughuli za kuendeleza uislamu. Katika hili waislamu tunatakiwa kujinyoshea vidole kabla ya kuwanyoshea wengine,” alisema.

Awali Kaimu Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Aboubakar Chalamila alionesha kushangazwa kwake na namna wakristo wanavyoisambaza dini yao kwa kasi kubwa tofauti kabisa na waislamu.

Akitoa mfano, Sheikh Chalamila alisema; “lipo dhehebu jipya kabisa la kikristo mkoani Iringa, dhehebu la Orthodox, nadhani halina zaidi ya miaka kumi lakini lina makanisa 37 katika maeneo mbalimbali ya mkoa wetu.”

Wakati kanisa hilo la mfano likikua kwa kasi kubwa, alisema kasi ya waislamu kusambaza dini yao na kuhakikisha huduma zake zinakuwa jirani na mazingira yao ni ndogo.

“Mfano taasisi hii ya Dhi Nureyn inayofanya kazi kwa kutegemea zaidi nguvu za wahisani toka nje, tangu ianzishwe  miaka 29 iliyopita imejenga misikiti 150 katika maeneo mbalimbali nchini. Misikiti hiyo ingekuwa imejengwa mkoani Iringa pekee tungesema ni mingi lakini kwa kuwa ni nchi nzima ni michache sana kulingana na mahitaji ya kusambaza uislamu kila mahali,” alisema.

Awali Katibu Mtendaji wa taasisi hiyo, Elm Shamsi alisema utegemezi wa misaada ya wahisani hasa wa nje ni changamoto inayosababisha taasisi kukosa chanzo endelevu cha mapato kwa ajili ya maendeleo ya dini hiyo.

Katika kuutekeleza mpango mkakati huo, alisema taasisi inatarajia wadau na jamii inayolengwa watachangia.

Alisema katika kila idara mkakati umelanga kufanikisha mambo makuu matano ambayo ni uzalishaji mali, kujitangaza, tathimini na ufuatiliaji, mafunzo na kuimarisha ushirikiano  na wadau wengine.

Mbali na Sh Milioni moja iliyochangwa na mjumbe huyo wa NEC, waumini wengine walioshiriki uzinduzi huo waliichangia taasisi hiyo Sh 348,000.
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.