WASANII WAANZA KUPAMBA UCHAGUZI 2015


Kampeni ya wasanii wa muziki wa kizazi kipya inayoitwa ‘Tuonane Januari’ inazidi kupamba moto na wiki hii jumla ya wasanii 10 watapanda jukwaa moja jijini Mwanza kwa kazi moja tu, kuwaambia vijana wenzao kushiriki katika zoezi la kujiandikisha daftari la wapiga ili kuleta mabadiliko katika uchaguzi wa mkuu ujao.
Kampeni hii imekuja baada ya kubainika kwamba vijana wengi ni waongeaji wazuri wa kwenye majukwaa na kila kukicha hulalamika kuhusiana na jinsi maendeleo ya nchi yanavyochelewa lakini unapofika wakati wa kupiga kura hawajitokezi au wanashindwa kupiga kura kutokana na kutokuwapo kwenye orodha.
Habari za ndani kutoka kwa wahusika wakuu wa kampeni hiyo inayohamasisha vijana kujitokeza kupiga kura na kuchagua viongozi vijana, bila kujali itikadi za vyama vyao, kufikia wiki ijayo itakuwa inageuza mwelekeo kwa kuweka hadharani, nani na nani wataanza kuungwa mkono na kundi hilo la wasanii kumi, watayarishaji wawili wa muziki na wadau mbalimbali.
Dhana nzima imekuja kwa kutokana na nguvu ya vijana, ambao wametajwa kuwa ndiyo nguzo ya mabadiliko iwapo wataamua kubadilisha fikra zao na kushiriki kikamilifu kwenye hatua muhimu za mabadiliko ya uongozi wa taifa lao, huku lengo kuu likiwa ni kuweka viongozi wa kisasa wenye mwelekeo wa kitaifa zaidi na siyo wa kisiasa.
Kwa wiki ya tatu mfululizo sasa, hili limekuwa somo linalotolewa kila kukicha, katika viwanja mbalimbali vya wazi, ambako kampeni hizi zinaendeshwa, huko, muunganiko wa wasanii na watayarishaji wa muziki hufanya mikutano inayoambatana na maonyesho ya bure, ikiwa ni sehemu ya kwanza ya kampeni kubwa itakayohimiza vijana kushiriki uchaguzi mkuu ujao ili kuweza kuchagua viongozi hasa vijana na wale wenye mitazamo chanya kwa maendeleo ya Tanzania.
Akiongea mbele ya umati wa vijana wapatao 10,000 waliohudhuria onesho la pili kufanyika nchini, lililofanyika Jumanne ya wiki hii viwanja vya sabasaba mjini Morogoro, Msanii Zuwena Mohamed `Shilole’, amesema baada ya miaka 50 ya kutawaliwa kisiasa baada ya Uhuru sasa ni wakati wa kuwa na uongozi wa kisasa ambao hautajali kiongozi ametoka chama gani, ili mradi tu awe kijana au kiongozi mwenye sifa za kuwa kiongozi bora, umoja huo umeahidi kuwaunga mkono watu wa namna hii.
“Ni wakati sasa wa kuachana na siasa, kudanganywa kila siku tumechoka, na kiukweli katika nchi hii vijana ndiyo wengi na tuna nguvu, hivyo tukiamua kuibadilisha nchi kwa nia njema tunaweza”, alisema Shilole.Kwa upande wake Nickson Simon, maarufu kwa jina la Nikki wa Pili kutoka katika kundi la Weusi alisema siasa ni jinamizi lililowagawa vijana kwa muda mrefu na kusababisha wakose umoja na kuwa na kauli moja kwa masilahi ya nchi. Pia, wao kama wasanii wameligundua hilo na wameamua kujitolea kutoa elimu kwa makundi ya vijana, na kuliweka pembeni na kuangalia mustakabali wa nchi.
“Kilichopo hapa vijana wenzangu ni kupiga chini siasa na kukubali usasa, tuangalie viongozi vijana wenye akili, tuachane na hivi vyama vinatupoteza,” alisisitiza Nikki.
Kampeni za Tuo8 Januari, zilianza wiki mbili zilizopita na zilizinduliwa Idara ya Habari Maelezo, huku msanii Fareed Kubanda akiwa kiongozi wa kampeni hiyo na tamasha la kwanza lilifanyika Jumapili ya tarehe 14, Desemba mwaka huu, katika Viwanja vya Sabasaba, mjini Njombe. Kwa mujibu wa Kubanda, kampeni hizi zinatarajiwa kuzunguka nchi nzima na kuanzia mwezi wa kwanza, muunganiko huo huenda ukaanza kutaja viongozi ambao wataanza kuwaunga mkono katika kampeni zao.
Mpaka sasa kampeni hiyo inajumuisha jumla ya wasanii 10 ambao wameamua kuzunguka nchi nzima kuhamasisha vijana wenzao kuleta mabadiliko ambao ni MwanaFA, Ditto, Fid Q, Nikki wa Pili, Shilole, Mwasiti, Linah, Godzilla, G Nako na Stamina.Wadau wengine wanaoshiri.ki kampeni hizi kwa kujitolea ni Watayarishaji P Funk na Lamar, pamoja na wadau Said Fela na Babu Tale.
Harakati ya Tuo8 Januari hazijafunga milango na wasanii wengine wataendelea kujiunga katika kampeni hizi.
Wiki ijayo wanatazamia kuwa Mwanza siku ya Jumapili tarehe 28-Desemba-2014.
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.