Maalim ajivua lawama Zanzibar
Sasa ni dhahiri. Mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad, ametabiri hatari ya mgawanyiko unaoweza kuikumba Zanzibar, lakini asingependa alaumiwe kwa uamuzi utakaochukuliwa Zanzibar.

Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) na Serikali ya Mapinduzi wametangaza kurudia uchaguzi Machi 20, mwaka huu.
Wakati kiongozi huyo wa CUF akitabiri mabaya, kwa upande wake amejivua lawama kwa lolote linaloweza kutokea kwa kuwa hajahusika kupanga programu yoyote licha ya kwamba yeye ni mmoja wa viongozi wakuu wa Serikali ya Mapinduzi.
Maalim Seif amekiri na kuiambia JAMHURI kuwa amefanya mawasiliano na mabalozi kadhaa na viongozi wa kimataifa juu ya hali ya siasa Zanzibar, na kusema: “Kwa hatari yoyote nisihusishwe. Naipenda Zanzibar, Wazanzibari wanajua hivyo, lakini watu wa CCM na Serikali yao wana yao.”
Anasema: “Nimewaambia mabalozi na marais wa nchi nyingi tu nimewaandikia kwamba nisingependa kuingizwa kwenye lawama kwa chochote kitakachojiri Zanzibar.”