CHADEMA KUPINGA MATOKEO MAHAKANI



Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wilaya ya Mpwapwa, mkoani Dodoma, kinapanga kwenda mahakamani kupinga matokeo ya ubunge na udiwani kwa baadhi ya kata  katika majimbo ya Mpwapwa na Kibakwe, kwa madai kuwa uchaguzi uligubikwa na rushwa na ukiukwaji wa taratibu na sheria.
 
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Katibu wa Chadema wilayani humo, Fabian Moke, alisema  kutokana na hali hiyo chama hicho kinajiandaa.
 
kwenda mahakamani kupinga matokeo hayo. Alisema kufuatia kasoro hizo, wagombea  wote wa  chama hicho katika maeneo hayo waligoma kusaini matokeo kutokana na  kutoridhishwa na mwenendo wa uchaguzi. “Tumeitisha  kikao cha dharura  cha viongozi ngazi ya wilaya na jimbo ili kueleza hali hiyo ya sintofahamu  kwa  wanachama wetu,” alisema Moke.
 
Hata hivyo, msimamizi wa uchaguzi  wilayani humo, Mohamed Maje, alisema sheria ya uchaguzi haikatazi kutangaza matokeo hata kama mgombea kagoma kusaini, bali anachotakiwa kufanya mgombea huyo ni kufuata taratibu za kisheria kutafuta haki yake.
 
Katika uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 25, mwaka huu, George Lubeleje (CCM) aliibuka mshindi wa nafasi ya ubunge Jimbo la Mpwapwa kwa kupata kura 32,208 sawa na asilimia 74.46, huku nafasi ya udiwani CCM ikishinda kata zote 15.
 
Kwa upande wa Jimbo la Kibakwe, George Simbachawene (CCM) ambaye pia ni Waziri wa Nishati na Madini, alitangazwa  mshindi wa nafasi hiyo kwa kupata kura  37,327 sawa na asilimia 81, huku kwenye udiwani CCM kikishinda viti vyote 18.
CHANZO: NIPASHE
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.