Kumbe Ngasa hapati chochote yanga alia njaa tu mtaaani

10th February 2015
Mshambuliaji wa Yanga, Mrisho Ngasa.
Baada ya kuifungia timu yake mabao yote katika ushindi wa 2-0 dhidi ya Mtibwa Sugar juzi, mshambuliaji wa Yanga, Mrisho Ngasa, amesema anajuta kuikataa ofa ya El Merreikh ya Sudan ambayo ilitaka kumsajili mwaka 2012.
 
Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Sudan na Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati walimuhitaji Ngasa kwa dau la Dola za Marekani 150,000 (Sh. milioni 269), lakini Ngasa chini ya ushawishi wa viongozi wa Yanga alikataa ofa hiyo na kurejea Jangwani baada ya mkataba wake wa mkopo wa kuichezea Simba kumalizika.
 
Ngasa ametoa kauli hiyo kufuatia kukatwa "fedha zote za mshahara" kwa ajili ya kulipia deni la Sh. milioni 45 ambazo alikopa benki mwaka jana.
Akizungumza jana na gazeti hili, Ngasa, alisema kuwa kwa sasa makato hayo yanamuumiza lakini hana la kufanya.
 
Alisema katika maafikiano, Yanga walimwambia watamkata Sh.500,000 kwa mwezi lakini ghafla walikiuka makubaliano na kuanza kumkata Sh. milioni moja kabla ya miezi miwili iliyopita kumkata pesa zake zote.  
 
Mshambuliaji huyo wa zamani wa Kagera Sugar ya mkoani Kagera na Azam ya jijini Dar es Salaam alisema kuwa anavumilia 'maumivu' hayo lakini bado anaamini milango ya yeye kwenda kucheza soka la kulipwa nje ya nchi bado haijafungwa kwa vile mkataba wake unaelekea kumalizika Yanga.
 
"Najuta kwa kukataa kwenda El Merreikh. Simba na Azam wanisamehe, walitaka kunipeleka huko lakini nilikataa na kwa mapenzi yangu nikaamua kurejea Yanga, sasa naumia, ila naamini kila jambo lina mwisho, deni nitamaliza kulilipa. Nilikopa mwenyewe na Inshallah nitamaliza kulilipa," alisema Ngasa.
 
Mshambuliaji huyo ambaye pia yuko katika kikosi cha timu ya soka ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars) na ambaye aliwahi kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa katika klabu ya West Ham United ya Uingereza na Vancouver Whitecaps ya Ligi Kuu ya Marekani akiitumikia klabu hiyo ya MLS katika mechi ya kirafiki dhidi ya Manchester United, alisema anaamini bado ana kiwango cha kucheza soka la kimataifa.
 
Aliongeza kwamba juhudi zake binafsi ndiyo zinamsaidia kuonekana mchezaji mzuri na ataendelea kujituma ili kutimiza ndoto zake.
 
Magoli hayo ya Ngasa yaliisaidia Yanga kulipa kisasi cha kufungwa 2-0 dhidi ya Mtibwa katika mechi yao ya mzunguko wa kwanza wa ligi kuu ya Bara na kupanda kileleni mwa msimamo wakiwa na pointi 25, tatu juu ya Azam walio na mechi mmoja mkononi.
 
Kikosi cha Yanga sasa kiko kambini kwa ajili ya kujianda na mechi yake ya hatua ya awali ya Kombe la Shirikisho dhidi ya BDF IX kutoka Botswana itakayofanyika Jumamosi Februari 14 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa.
 
CHANZO: NIPASHE 
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI 
Theme images by hanoded. Powered by Blogger.